Thursday 30 May 2013

SERIKALI IMESHINDWA KUDHIBITI BODABODA?

Kama kuna eneo ambalo Serikali imeonyesha udhaifu mkubwa ni udhibiti wa usafiri wa pikipiki, maarufu kama Bodaboda. Udhaifu huo umetoa mwanya kwa waendesha Bodaboda kuweka kando sheria za usalama barabarani na kufanya usafiri huo kuwa janga la kitaifa kutokana na kusababisha ajali zinazoua maelfu ya watu kila mwaka, huku maelfu ya majeruhi wakiwa wamepoteza viungo muhimu katika miili yao.
Licha ya Jiji la Dar es Salaam kuwa machinjio makuu ya wahanga wa ajali hizo, tatizo hilo limeikumba Tanzania Bara kuanzia kata hadi makao makuu ya mikoa. Waendesha Bodaboda na abiria wao wanakufa ovyo kila siku katika ajali. Serikali imebaki kuwa mtazamaji na kujivua jukumu la kuhakikisha kwamba inalinda maisha ya raia wake.
Taarifa za Jeshi la Polisi zimethibitisha kuwapo watu wengi wanaopoteza maisha na wengine kujeruhiwa vibaya katika ajali hizo, hivyo kupoteza rasilimali kubwa kwa maendeleo ya nchi yetu. Kwa mfano, takwimu za ajali hizo mkoani Dar es Salaam zinatisha. Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohamed Mpinga amesema watu 1,875 walikufa jijini katika kipindi cha 2011/12 kutokana na ajali za barabarani, ikiwa ni wastani wa vifo vya watu watatu kila siku. Takwimu za 2012/13 bado zinakusanywa, lakini jeshi hilo linasema idadi ya watu waliokufa nchi nzima tangu mwanzoni mwa mwaka huu ni kubwa mno ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka uliopita. Madaktari na wauguzi wamesema wameelemewa na idadi kubwa ya majeruhi hao. Wengi wamepoteza viungo muhimu, hivyo wamebaki kuwa tegemezi. Wamekata tamaa. (www.mwananchi.co.tz)

No comments:

Post a Comment