Thursday 30 May 2013

TCRA kuanza udhibiti rasmi wa namba za simu nchini kesho

Dar es Salaam. Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kesho inaanza kudhibiti namba za simu za mikononi mpya na zisizosajiliwa kwa kuzifungia. Pia imeishauri Serikali kuongeza kasi katika utoaji wa vishambulisho vya taifa ili viweze kutumika kuwatambua wahalifu .
Akizungumza jana Dar es Salaam, Mkurugenzi wa TCRA Profesa John Nkoma alisema kuwa hatua hiyo imelenga katika kuhakikisha kwamba inawadhibiti wateja wapya kutotumia namba hizo kabla ya kujisajili.
“Kuanzia June Mosi mwaka huu (kesho),hakuna mtu anayeweza kununua kadi ya namba za simu na kuitumia siku hiyo hiyo. Kuna utaratibu maalumu umewekwa,.Pia kwa wateja wengine tumewapa nafasi ya kuhakikisha wanajisajili na tumeongeza muda hadi Julai 10 wasipojisajili tutawafungia rasmi,” alisema Profesa Nkomwa.
Akifafanua zaidi juu ya msimamo huo Profesa Nkoma alisema ni kosa la jinai kutumia namba ya simu isiyosajiliwa na adhabu yake ni faini ya Sh500,000 au kifungo cha miezi mitatu jela.
Akijibu lawama zinazoelekezwa kwa TCRA kwa kushindwa kudhibiti matumizi ya simu kwa njia ya usajili, alisema kumekuwa na tatizo linalotokana na baadhi ya wahalifu kugushi kwa kuandika taarifa za uongo na picha zisizowahusu.
Alisema pia kuna haja ya watu kubadili tabia kwa kuwaripoti watu wanaofanya matukio ya uhalifu yanayohusisha simu za mkononi hasa wizi au lugha chafu, udanganyifu na usaliti.
“Simu naweza kuifananisha na kisu. Kinasaidia kama matumizi ni mazuri, lakini mhalifu anaweza kukitumia kudhuru,”alisema Prof.
Profesa Nkoma.

No comments:

Post a Comment